R.C ANDENGENYE AIPONGEZA KIGOMA D.C KWA HATI SAFI-ASISITIZA USIMAMIZI THABITI MAPATO YA NDANI

Mkuu wa Mkoa wa Kigoma Mhe.CGF(Rtd) Thobias Andengenye ameipongeza Halmashauri ya Wilaya ya Kigoma kwa kupata hati safi kutoka ofisi ya Mdhibiti Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali huku akisisitiza usimamizi thabiti wa Mapato ya Ndani.
Mhe.Andengenye ametoa kauli hiyo leo tarehe 14 Juni,2025 wakati wa Kikao Maalum cha Baraza la kujadili hoja na Mapendekezo ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kilichofanyika katika ukumbi wa Halmashauri ya Wilaya uliopo eneo la Mahembe.
"Mwisho wa Ukaguzi mmoja ni mwanzo wa Ukaguzi unaofuata,hivyo niwasihi Wakuu wa Idara na Vitengo mjipange kwaajili ya Ukaguzi unaokuja,haya Mafanikio ya kupata hati inayoridhisha lazima tuyalinde kwa wivu mkubwa"amesisitiza Mhe.Andengenye
RC Andengenye amesema "Tunatafuta vyanzo vipya vya Mapato na kutanua wigo,lakini pia baada ya kupata ni lazima tuhakikishe hizo fedha zilizopatikana hazipotelei kwenye mifuko ya watu binafsi, kwahiyo lazima tuzuie mianya yote ya upotevu wa mapato".amesema Mhe.Andengenye
Naye Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Kigoma Mhe.Joseph Nyambwe amebainisha namna ambavyo Halmashauri imepiga hatua kubwa kwenye ukusanyaji wa mapato ya ndani kutokana na ushirikiano baina ya Waheshimiwa Madiwani na Mkurugenzi Mtendaji pamoja na wataalam.
Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Kigoma Mwl.Chiriku Hamisi Chilumba amemhakikishia Mkuu wa Mkoa kuwa maelekezo yote yaliyotolewa katika kikao hicho yatazingatiwa na kufanyiwa kazi kwa ukamilifu kadiri inavyopasa.
Kikao hicho kimehudhuriwa na Katibu Tawala wa Mkoa wa Kigoma Mhe.Hassan Rugwa pamoja na Katibu Tawala wa Wilaya ya Kigoma Mganwa Nzota kwa niaba ya Mkuu wa Wilaya ya Kigoma pamoja na Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Mkoa wa Kigoma.