DAS NZOTA APIGA MARUFUKU MASOKO YA USIKU KWA WATOTO WA UMRI WA CHINI YA MIAKA 18

Katibu Tawala wa Wilaya ya Kigoma Mhe.Mganwa Nzota amewapiga marufuku Wazazi wanaowatuma watoto wao walio chini ya umri wa miaka 18 kufanya Biashara kwenye masoko ya usiku ili kuwaepushia vitendo vya ukatili wa kijinsia.
DAS Nzota ametoa mwito huo leo tarehe 16 Juni,2025 wakati wa Maadhimisho ya Siku ya Mtoto wa Afrika yaliyofanyika katika viwanja vya Shule ya Msingi Kagina katika Kata ya Kagongo kwenye Halmashauri ya Wilaya ya Kigoma.
"Tambueni watoto wote wanaohusishwa kwenye masoko ya usiku ili Wazazi wao tuweze kuwachukulia hatua za kisheria,tukibaini mtoto yuko sokoni usiku katika wakati ambao anatakiwa ajisomee,mchukueni mtoto huyo mpaka nyumbani kwao na Wazazi wake tumchukulie hatua za kisheria"amehimiza DAS Nzota
Amesema tukiweza kudhibiti jambo hilo watoto wataweza kupata muda mzuri wa kujisomea na kupunguza wigo wa vitendo hatarishi ambavyo mtoto anaweza kukutana navyo katika mazingira ya masoko ya usiku yanayodumu hadi muda wa usiku mkubwa.
Aidha DAS Nzota amewasisitiza wazazi kutenga muda wa kutosha wa kuwasikiliza watoto wao na kusikiliza changamoto wanazozipitia ili kupunguza matendo ya Ukatili wa kijinsia kwa watoto kwa kuwalinda watoto huku akihimiza kuwa jukumu la kwalinda watoto ni jukumu la jamii nzima.
Amesema jitihada zinazofanywa na Serikali za kuboresha huduma za Afya na Elimu zinapaswa kuungwa mkono na Mzazi mmoja mmoja kwa kuchangia michango itakayowawezesha watoto kupata huduma za msingi ili waweze kufikia ndoto zao siku za usoni.
Chimbuko la Maadhimisho ya Siku ya Mtoto wa Afrika hutokana na mauaji ya watoto zaidi ya Elfu 2 yaliyofanywa na utawala wa Makaburu katika Kitongoji cha Soweto nchini Afrika Kusini tarehe 16 Juni,1976 ambapo kwa mwaka huu Maadhimisho hayo yamebeba Kaulimbiu isemayo "Haki za Mtoto,tulikotoka,tulipo na tunakoenda'